Mkuu
 wa Wilaya ya Kinondoni, Mh Ally Hapi leo ametengua uteuzi wa aliyekuwa 
Kaimu Mganga Mkuu Mfawidhi wa Hospitali ya Mwananyamala Dkt. Delila 
Mushi kwa kosa la kupandisha bei ya baadhi ya huduma kinyume cha 
taratibu na sheria.
Mushi
 amedaiwa kupandisha bei ya huduma hizo baada ya kukaa kikao cha 
hospitali pasipo kuipeleka hoja ya kupandisha bei katika kikao cha Idara
 ya Manispaa na huduma za jamii.
Taratibu
 alizotakiwa kufuata Mushi ni kuipeleka hoja hiyo Manispaa, ambapo 
ingejadiliwa kwenye kikao cha huduma za jamii kisha baraza la madiwani 
kuipitia na kuitolea maamuzi jambo ambalo hakulifanya badala yake 
alipandisha bei pasipo kupitia taratibu hizo.
Bei
 ya huduma zilizopandishwa ni pamoja na bei ya kadi  ambapo wagonjwa 
waliofika katika hospitali hiyo bila ya barua ya rufaa kutoka vituo vya 
afya na zahanati zilizo karibu nao, walitakiwa kulipa sh 10,000 badala 
ya 6,000.
“Hakuna
 jambo baya kama kiongozi kufanya maamuzi pasipo kufuata utaratibu 
halafu maamuzi hayo yakaathiri wananchi wanyonge, mkurugenzi nakuagiza 
hiyo bei ya kadi irudi kama ilivyokuwa awali, huwezi mlipisha mgonjwa 
kiasi kikubwa cha fedha huku huduma unazotoa haziendani na bei hiyo, ” amesema Hapi.
“Hakuna
 sababu ya anayekaimu nafasi ya mganga mkuu kwa sasa kubaki na wadhifa 
huo wakati haumtoshi, atatafutwa mwIngine kuja kuwa mganga Mkuu, ” amesema.
Kwa sasa ameteuliwa Dkt. Daniel Nkungu kukaimu kwa muda wadhifa huo hadi atakapoteuliwa mganga mwingine kushika wadhifa huo.
Hata
 hivyo, Baada ya Hapi kutoa agizo la kutenguliwa uteuzi wa Dkt. Mushi na
 kuamuru Wagonjwa kulipa bei ya kadi ya awali, baadhi ya wahudumu wa 
mapokezi waligoma kutoa huduma kwa madai kuwa mifumo ya utoaji risiti 
imeharibika.
Mariam Hamisi Sahabani mkazi wa Kinondoni, alifafanua jinsi wahudumu hao walivyogoma baada ya mkuu wa wilaya kuondoka.
“Baada
 ya Mheshimiwa kuondoka wamegoma kutoa huduma kwa kigezo kuwa mashine 
ilikuwa mbovu, inawezekanaje? Mbona wakati tunalipa 10,000 mashine 
zilifanya kazi, iweje sasa zisifanye? ” alihoji.
Kufuatia
 malalamiko hayo yaliyotolewa na wananchi waliokuwepo kwenye hospitali 
hiyo, Mganga mkuu wa Manispaa ya Kinondoni Dkt. Aziz Msuya alisema 
atawasimamisha kazi waliogoma kutoa huduma kwa kuwa walikuwa na lengo la
 kupinga kauli ya serikali.
“Naagiza huduma ianze kutolewa kuanzia sasa, na watakaogoma kutoa huduma nitawasimamisha kazi kuanzia kesho, ” amesema Msuya.
 

 
Post a Comment Blogger Facebook