Wakati
 mgombea Urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), John Magufuli, 
akitarajiwa kuzindua kampeni zake kesho jijini Dar es Salaam, mgombea 
kupitia Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), Edward Lowassa amekwama 
kuzindua kampeni zake  kama ilivyotangazwa awali.
Ukawa
 unaoundwa na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), National 
Convention for Construction and Reform – Mageuzi (NCCR-Mageuzi), Chama 
cha Wananchi (CUF) na National League for Democracy (NLD) umeahirisha 
uzinduzi kutokana na kukosa mahali patakapotosha ‘mafuriko’ ya watu 
watakaohudhuria.
Lowassa
 alitarajiwa kufungua pazia kwa kuzindua kampeni zake kwenye Uwanja Mkuu
 wa Taifa jijini Dar es Salaam, lakini serikali imekataza uwanja huo 
kutumika kwa kampeni za vyama vya siasa.
Mkurugenzi
 wa Idara ya Habari (Maelezo), Assah Mwambene, akiongea na waandishi wa 
habari Jumatano wiki hii, alisema serikali imefikia hatua hiyo kwa vile 
kusudio la ujenzi wa uwanja huo ni shughuli za michezo pekee na si 
vinginevyo. 
Kampeni
 zinazoanza kesho  pia zitahusisha wagombea urais kupitia vyama vingine 
vya siasa vikiwamo ambavyo wagombe wake hawapewi nafasi kubwa ya kuibua 
ushindani kama itakavyokuwa ama kukaribia kwa CCM na Ukawa.
Pia kuanza kwa kampeni hizi kutawahusisha wagombea ubunge na udiwani watakaoshiriki Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 25, mwaka huu.
Afisa
 Habari wa Chadema iliyo mshirika katika Ukawa, Tumaini Makene, amesema 
kuwa, Lowassa anayewania Urais akiwa na mgombea mwenza Juma Duni Haji, 
ameahirisha kuzindua kampeni zake mpaka itakapotangazwa baadaye.
Alisema
 kuahirishwa kwa uzinduzi huo kunalengo la kutoa fursa kwa Ukawa 
kujiweka sawa hasa katika kupata uwanja wenye uwezo wa kuwajumuisha watu
 wengi na nafasi za kuegesha magari.
“Mgombea
 wetu hatazindua kampeni leo wala kesho, waache hao wengine waanze sisi 
tunajipanga kupata eneo zuri litakalotosha kwa idadi kubwa ya watu 
tunaowatarajia ikiwamo na maegesho ya magari,” alisema.
Makene
 alisema kutokana na uzeofu uliojionyesha wakati mgombea wao akitafuta 
wadhamini ama kutambulishwa mikoani, wanaamini kuwa mkutano wao 
utahudhuriwa na watu wengi, hivyo ni muhimu wakatafuta eneo kubwa la 
kutosha watu wengi na maegesho ya vyombo vya usafiri.
Wakati
 ikitarajiwa kuzindua kampeni zake kesho, CCM imeshatangaza kamati ya 
watu 32 kwa ajili ya kutafuta ushindi, ikiongozwa na Katibu Mkuu wa 
chama hicho, Abdulrahaman Kinana.
Kamati
 hiyo ilitangazwa na Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye, 
Jumanne  wiki hii ambaye alimuita Kinana kama mwanaharakati wa kivita 
anayefahamu medani za ushindi.
Uchaguzi
 wa mwaka huu ambao unatarajiwa kuwa na changamoto kubwa hasa kutokana 
na mgombea anayeungwa  mkono na Ukawa (Lowassa) akitokea CCM, kuonyesha 
upinzani mkubwa dhidi ya  CCM alichokuwa mwanachama wake tangu mwaka 
1977.
Licha
 ya kuwa mwanachana, Lowassa ameshika nafasi tofauti ndani ya CCM na 
serikalini ikiwamo Uwaziri Mkuu aliojiuzulu mwaka 2008.
Lowassa
 alikuwa pia katika timu ya kampeni za mwaka 2005 ambapo Rais Jakaya 
Kikwete aliwania nafasi hiyo kwa mara ya kwanza na kupata ushindi wa 
kishindo.
Hata
 hivyo, Julai 29, mwaka huu, Lowassa aliamua kujiunga na Chadema ikiwa 
ni siku chache baada ya jina lake kukatwa katika hatua za awali za 
kuwachuja watia nia waliotaka kuwania Urais kupitia CCM.
Jumla
 ya makada 42 wa CCM walijitokeza kwenye kinyang’anyiro cha kumtafuta 
mgombea urais ambapo 38 walirejesha fomu na Magufuli aliibuka kuwa 
mshindi atakayegombea Urais katika ‘kumrithi’ Rais Kikwete.
Macho
 na masikio ya wapiga kura wengi kuanzia kesho yataelekezwa kwenye 
uzinduzi wa kampeni hizo kusikia sera za vyama hivyo vikubwa 
vinavyoshindana kumpata Rais wa awamu ya tano wa Jamhuri ya Muungano wa 
Tanzania.
Post a Comment Blogger Facebook